Kavazi la Dkt. Salim: Jenerali Ulimwengu na Gazeti la Rai mwaka 1995

Na Mohamed Said
KATIKA Kavazi la Dk. Salim Ahmed Salim anaeleza simu aliyopigiwa na Jenerali Ulimwengu tarehe 29 Machi 1995 na walizungumza kuhusu Burundi, siasa za Tanzania na Uchaguzi Mkuu wa mwaka huo.
Mimi nilivutiwa na hili la Uchaguzi Mkuu wa 1995 kwa kuwa kwa njia moja au nyingine nilihusika na nilikuwa kama alivyokuwa akifanya Salim kuweka shajara (diary) nami pia nikifanya hivyo kwa yale niliyoshiriki.
Salim anasema mazungumzo yao ghafla yaliingia katika Uchaguzi Mkuu. Siwezi kueleza aliyoandika Salim lakini kitu ambacho kiliniburudisha kwanza ni ujuzi wake wa lugha ya Kiingereza na pili Salim anachagua maneno yake kwa utaalamu wa hali ya juu mno.
Ili kumweleza nini khasa anasema inabidi msomaji ufanye kazi ya ziada kwa kutembea katikati ya mistari. Hii si kazi ndogo na inaendana na kitu kinachoitwa kuelewa ”difficult passages,” na hili ni somo maalum. Salim nathubutu kusema kabobea katika fani hii.
Salim anahitimisha kwa kusema siku ya pili baada ya mazungunzo yake na Jenerali Ulimwengu taarifa zikamfikia Addis Ababa kuwa habari kuu ukurasa wa mbele wa gazeti la Rai Mhariri wake akiwa Jenerali Ulimwengu limeandika, ‘’Salim si mgombea lakini…’’
Haraka nikashuka kwenye notes zake.
Hapa kwa mara ya kwanza nakutana na maajabu ambayo mtu usihadithiwe unataka uone kwa macho yako mwenyewe. Katika uzinduzi wa Kavazi la Dk. Salim, Prof. Saida Yahya alieleza kuwa Salim anaweka notes zake akianza na tarehe, saa na dakika ya tukio nk.
Naam nimekutana na ukweli huu na kushuhudia kwa macho yangu.
Lakini hili si lililonishtua sana.
Lilonifanya moyo wangu ubadili mapigo ni pale niliposoma Dr. Salim anaeleza kuhusu ujumbe aliopelekewa kutoka Geneva na Balozi Khamis Suedi, kutoka kwa Hamza Aziz, Idi Simba, Abbas Sykes na Balozi Abdallah Suedi.  Hawa wote waliotajwa hapo nilipata kufanyanao mazungumzo nyumbani kwa Abbas Sykes, Sea View ambako alinialika chakula cha mchana na hawa wazee wangu walikuwapo pamoja na Ahmed Rashaad Ali. Mazungumzo yetu yalikuwa kuhusu Uchaguzi Mkuu na wazee wangu walitaka kujua Waislamu wana msimamo gani?
Miaka mingi imepita.
Haraka sana nikaingia Maktaba na kutoa shajara yangu ya mwaka wa 1995 nikafungua mwezi March kuangalia nimeandika nini.
Kipindi hicho joto la Uchaguzi Mkuu lilikuwa juu sana. Gazeti la Serikali Daily News ukurasa wa mbele katika wino mweusi uliokoza kulikuwa na kichwa hiki cha habari: ‘’Sendoro Speaks on Election.’’ Elinaza Sendoro alikuwa Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT).  Sendoro alikuwa anaonya kuhusu siasa kali na kuwa kura zitapigwa kwa kuangalia dini na sio uwezo wa wagombea na akatoa wito wa kuepuka uwezekano wa Tanzania kugawanyika katika kambi mbili zinazokinzana.
Shajara yangu inanieleza kuwa nilikuwa na mazungumzo na Prof. Haroub Othman na akanieleza kuwa Dr. John Sivalon alikuwa anataka kufanya semina kuhusu ‘’Dini na Siasa’’ kwa kuwa Uchaguzi Mkuu utatawaliwa na udini. Semina hii haikuweza kufanyika kwa kuwa wahisani hawakupendezewa nayo lakini walikuwa tayari kutoa fedha kiandikwe kitabu.
Prof. Haroub Othman akaniambia kuwa yeye amewaomba Dr. Khalfan na Dr. Sivalon wote kutoka Chuo Kikuu Cha Dar-es-Salaam kuratibu mradi huo na mimi niandike moja ya sura katika kitabu hicho.
Haya ndiyo niliyoandika tarehe 1 Machi.
Machi 2 sentensi ya kwanza niliyoandika ni Adam Lusekelo akitangaza kupitia BBC Idhaa ya Kiswahili kuwa Augustino Mrema amejitoa CCM. Machi 3 Rais Mwinyi akizungumza katika Eid Baraza iliyoandaliwa na BAKWATA Ukumbi wa Diamond Jubilee aliwaonya Waislam kutosababisha kuvunjika kwa amani.  Mwinyi, kwa bahati mbaya sana, kwa kutoijua historia ya uhuru wa Tanganyika alidhani kuwa kwa kuwafokea Waislamu yeye atapendeza na kupendwa.
Haikuwa hivyo.
Augustino Mrema kwa mambo aliyokuwa akifanya alionekana ana nguvu kumshinda Rais Mwinyi. Siku tatu kabla ya Mrema hajajitoa CCM, John Bwire mmoja wa wahariri wa Rai akihojiwa na BBC Idhaa ya Kiswahili alisema kuwa Mrema alikuwa kipenzi cha wananchi wa mji huo na wakimzunguka kwa mapenzi makubwa kila alipojitokeza hadharani.
Haya hayakuwa bure kulikuwa na ujumbe maalum katika yote haya na wenye macho waliona na wenye masikio walisikia. Katika Sala ya Ijumaa Msikiti wa Mtoro siku hiyo hiyo Sheikh Khalifa Khamis alimshambulia sana Augustino Mrema. Kila kukicha asubuhi kuna jipya.
Machi 4, gazeti la Nipashe likaandika katika ukurasa wa mbele kuwa Sheikh Mkuu wa BAKWATA Sheikh Hemed bin Jumaa amewaonya Waislam wasiwapigie kura Waislam wenzao katika uchaguzi utakaofanyika Oktoba.
Hii ndiyo hali ya siasa iliyokuwapo wakati nilipokutana na wazee wangu wale nyumbani kwa Balozi Abbas Sykes wakaniuliza Waislamu wana lipi katika uchaguzi unaokuja mwezi October 1995.
Mazungumzo yetu yalikuwa marefu na nakumbuka Mzee Rashaad mbele yao alikuwa akiniambia, “Mohamed hapa uko ndani ya kambi ya adui haya yote unayowaeleza yatafika Makao Makuu Dodoma.” Si kama sikuyajua hayo lakini nilitaka kufikisha ujumbe.
Nilipomaliza kumsoma Dk. Salim nikajiuliza kwa nini ilikuwa lazima ielezwe au ienezwe na Rai kuwa Salim Ahmed Salim si mgombea wa nafasi ya urais kwa tiketi ya CCM?
Je, hii ilikuwa moja ya njia ya kumsafishia njia Benjamin Mkapa?
Ieleweke kuwa Mkapa na Jenerali Ulimwengu walipata kuwa marafiki wakubwa.
Nikajiuliza tena kuna uwezekano kuwa yale ambayo niliwaeleza wazee wangu siku ile pale nyumbani kwa Balozi Sykes ndiyo huu ujumbe uliotoka kwa Balozi Khamis Suedi Genava kwenda kwa Dk. Salim Ahmed Salim Addis Ababa?
Salim hakusema ule ujumbe ulikuwa wa nini. Kilichobakia ni dhana tu. Labda ilikuwa kuhusu Uchaguzi Mkuu.  Kavazi la Dk. Salim lina mambo hapana mchezo.
Allah Ndiye Mjuzi.